Papa Francis Afariki Dunia Akiwa na Umri wa Miaka 88
Tarehe: 21 Aprili 2025
Na: The Gurdian |AP NEWS | MY MEDIA
Papa Francis, kiongozi wa Kanisa Katoliki duniani, amefariki dunia leo Jumatatu ya Pasaka, tarehe 21 Aprili 2025, akiwa na umri wa miaka 88. Taarifa rasmi ya kifo chake imetolewa na Kardinali Kevin Farrell, Camerlengo wa Vatican, aliyethibitisha kuwa Papa alifariki saa 1:35 asubuhi kwa saa za Vatican.
Papa Francis, ambaye jina lake halisi ni Jorge Mario Bergoglio, alichaguliwa kuwa Papa mwaka 2013 na kuwa Papa wa kwanza kutoka Amerika ya Kusini pamoja na kuwa wa kwanza kutoka ndani ya Shirika la Kijesuiti. Alijulikana kwa maisha ya unyenyekevu, kujitoa kwa ajili ya maskini, na juhudi za kuleta mageuzi ya kijamii na kiroho ndani ya Kanisa Katoliki.
Katika miezi ya hivi karibuni, afya ya Papa Francis ilikuwa imedorora kutokana na matatizo ya kupumua na figo, ikiwa ni pamoja na nimonia kali. Alilazwa hospitalini kwa siku 38 kabla ya kuruhusiwa na kuonekana hadharani kwa mara ya mwisho Jumapili ya Pasaka, akiwa ameketi kwenye kiti cha magurudumu, huku akiwa katika hali dhaifu.
Kifo cha Papa Francis kimeacha pengo kubwa si tu kwa Kanisa Katoliki bali pia kwa ulimwengu mzima, ambao ulimtambua kama kiongozi wa kiroho aliyekuwa na msimamo wa haki, amani na mshikamano wa kijamii.
Vatican imetangaza kuwa maandalizi ya mkutano wa makardinali (conclave) kwa ajili ya kumchagua Papa mpya yataanza hivi karibuni.





